CCM; PINDA NA HAWA GHASIA WANG'OKE

CCM; PINDA NA HAWA GHASIA WANG'OKE

 
Rais Jakaya Kikwete, ameshauriwa kumng’oa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ikielezwa sababu kuwa ndiye kikwazo katika utendaji wa Serikali na kwamba akiachwa ataipeleka pabaya Serikali na CCM.
Kikwete pia ameshauriwa kumfukuza kazi Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia, kwa kushindwa kukabiliana na matatizo ya ubadhirifu katika halmashauri nchini.
“Kama (Rais) unaitakia mema nchi na CCM kuchukua hatua za kuwafukuza kazi Pinda na Waziri Ghasia,” alisema Mbunge wa Mwibara, Khangi Lugola (CCM), juzi alipochangia taarifa za Kamati za Bunge kuhusu hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30 mwaka jana.
“Kwa nini Watanzania wafe kwa kunyimwa misaada na wafadhili kwa sababu ya mtu mmoja tu Pinda, kwa ajili ya Ghasia ameiendesha Tamisemi kama Saccos ama Vikoba?” alihoji.
 “Mchawi wetu ... ni Waziri Mkuu Mizengo Pinda amekuwa mpole mno hawajibiki,” alisema Mh. Lugola na kuongeza, “Kuanzia jana (juzi) Waziri Mkuu anahudhuria mahafali.”
Wakati Lugola akizungumza mawaziri waliokuwepo bungeni ni wanne, manaibu mawaziri wawiliwawili, wakati  mawaziri wote 53.

India, Ufaransa, Marekani, Canada zaomboleza kipekee

 
Wakati Bara la Afrika likiendelea na maombolezo ya kifo cha aliyekuwa Rais wa kwanza wa Afrika Kusini na mkombozi aliyepinga siasa za ubaguzi za makaburu, Nelson Mandela, mataifa mengine duniani yameonyesha kufanya maombelezo katika namna mbalimbali.
Pamoja na kutuma salamu za rambirambi kwa familia ya Mandela na wananchi wa Afrika Kusini, viongozi wa mataifa makubwa duniani wameonyesha kuguswa na msiba huo kiasi cha kuomboleza kwa namna tofauti tofauti.
India
Hii inaweza kuwa ni nchi mojawapo ambayo imetangaza siku nyingi zaidi za maombolezo kwa ajili ya kifo cha Nelson Mandela kutoka nje ya Bara la Afrika.
Baada ya kupata taarifa za kifo cha Mandela, Serikali ya India kupitia Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Manmohan Singh aliwatangazia siku tano za maombelezo na kuamuru bendera zipeperushwe nusu mlingoti katika kipindi hicho cha maombolezo.
Sambamba na hilo, Singh  alimwelezea  namna kiongozi huyo wa Afrika alivyokuwa shujaa katika kupinga mfumo wa kibaguzi.
Ufaransa
Kuonyesha kuwa taifa hili pia limeguswa kwa kiasi kikubwa na msiba huu, jengo refu zaidi mjini Paris la Eiffel Tower liliwashwa taa zenye rangi zilizopo kwenye Bendera ya Afrika Kusini.
Picha zilizopigwa katika jengo hilo mpaka siku ya jana, linaionyesha likiwa limenakshiwa na taa zenye rangi tano  za bendera hiyo zikiwemo nyekundu, kijani, nyeusi, njano na nyeupe.
Marekani
Taifa hili lenye nguvu duniani limeonyesha heshima kubwa kwa Nelson Mandela kwa kupeperusha bendera zake nusu mlingoti nchi nzima na kuweka siku tatu za maombolezo.
Kana kwamba hiyo haitoshi taa zenye rangi ya Bendera ya Afrika Kusini zilionekana kung’arisha jengo la Empire state lililopo NewYork na Hoteli ya Omni iliyopo Dallas.
Mjini Washington jengo la Ubalozi wa Afrika Kusini lilitawaliwa na taa hizo pamoja na bendera za nchi hiyo hali iliyosababisha mwonekano wa eneo hilo kubadilika kabisa.
Pia  kiongozi wa taifa hilo Rais Barack Obama alifanya mazungumzo kwa njia ya simu na Graca Machel ambaye ni mjane wa Mandela.
Taarifa kutoka Ikulu ya Marekani ilisema kuwa Obama alimpigia simu mama Machel kwa lengo la kumtumia salama za rambirambi.
Canada
Kwa mujibu wa taarifa zilizoripotiwa na vyombo vya habari nchini Canada, Waziri Mkuu Stephen Harper amewaalika mawaziri wakuu wengine wastaafu wa nchi hiyo kuungana naye kuelekea Afrika Kusini kwa ajili ya mazishi ya Nelson Mandela.
Australia na Uingereza
Kama ilivyo kwa nchi nyingine, mataifa haya pia yalitangaza siku za maombolezo sanjari na kupeperusha bendera zake nusu mlingoti kuashiria maombolezo ya kifo cha kiongozi shujaa na mahiri barani Afrika, hayati Nelson Mandela.

Stars kuivaa Kenya nusu fainali

 
Mombasa. Ushujaa wa kipa namba moja wa Kilimanjaro Stars, Ivo Mapunda umeivua ubingwa Uganda na kuiingiza Stars nusu fainali ya Kombe la Chalenji.
Stars itacheza na Kenya iliyoilaza Rwanda bao 1-0 katika mechi nyingine ya robo fainali iliyochezwa jana jioni kwenye Uwanja huohuo wa Manispaa unaobeba mashabiki 15000.
Uganda iliutwaa ubingwa huo mwaka jana mjini Kampala ikiwa haijafungwa bao hata moja kwenye mechi zake zote, Uganda ilikuwa inaelekea kutimiza rekodi hiyo lakini jana Stars ikatibua mambo. Awali kwenye mechi za makundi Uganda ilikuwa haijaruhusu bao lolote.
Mapunda anayeichezea Gor Mahia ya Kenya alipangua penalti mbili za Uganda ambayo kocha wake, Sredejovic Milutin ‘Micho’ alijitetea kwamba penalti hazina ufundi na wala Stars haijafanya cha ajabu. “Hakuna cha ajabu kwenye penalti, hakuna fundi.”
Licha mwamuzi Msomali, Wish Wabarow kuonekana kuzidiwa na mchezo, mechi hiyo ilimalizika kipindi cha kwanza Stars ikiongoza mabao 2-1 huku ikishangiliwa na uwanja mzima uliokuwa umetawaliwa na Wakenya na Watanzania walioingia kupitia Lungalunga, Tanga.
Straika wa Uganda anayewindwa na Yanga, Danny Serunkuma ndiye aliyefunga bao la kwanza dakika ya 16 akipiga shuti kali katikati ya mabeki wa Stars lakini dakika mbili baadaye Mrisho Ngassa alisawazisha kwa shuti kali kutoka nje kidogo ya boksi likamshinda kipa Benjamin Ochan.
Ngassa huyohuyo akapiga bao la pili kwenye eneo lilelile dakika ya 38. Mchezo huo uligubikwa na aibu ya aina yake kutokana na kutokuwepo kwa wasaidizi wa Msalaba Mwekundu kwa kile kilichodaiwa kwamba hawajalipwa chao na Cecafa.
Timu hizo zilishambuliana kwa kasi kipindi cha kwanza ambapo mastraika Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu waliipa shida Uganda ambayo kwa siku ya jana straika wake, Danny Serunkuma ndiye aliyeisumbua zaidi Stars.
Kipindi cha pili dakika 52 Aboubakar Salum ‘Sure boy’ ambaye alikuwa akichezesha timu, alionyeshwa kadi nyekundu baada ya kumkanyaga beki wa kushoto wa Uganda, Godfrey Walusimbi.
Dakika ya 75 beki mrefu wa Uganda alifunga bao laini baada ya Ivo kuutema mpira wa kona ya Wakiro Wadada.
Baada ya kumalizika kwa dakika 90, zilipigwa penalti ambapo Uganda ilikosa tatu na Stars ikakosa mbili. Penalti za Stars zilipigwa na Erasto Nyoni na Mbwana Samatta (walikosa), Amri Kiemba, Athuman Idd na Kelvin Yondani. Uganda walipiga Danny Walusimbi (alikosa), Emanuel Okwi, Aucho Khalid (alikosa), Hamis Kiiza na Serunkuma aliyekosa penati ya mwisho na kuivusha Stars.
Ivo Mapunda ambaye alikuwa akishangiliwa na mashabiki wengi wa Kenya alisema: “Siamini kwamba tumeshinda, ni Mungu tu. Mpira ulikuwa mgumu sana na tulicheza na timu ngumu ambayo tumeitoa kwa juhudi binafsi za wachezaji.”

Jela ilivyokuwa ‘Chuo Kikuu’ cha Mandela

 
Juni 12, 1964, Nelson Mandela alihukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya kufanya hujuma dhidi ya Serikali ya kibaguzi ya Makaburu.
Hata hivyo Mandela alitumikia kifungo hicho kwa miaka 27 na kutoka akiwa mtu aliyebadilika kitabia, akiwa mtulivu, akiwa na hekima, mwenye busara na mwenye kuheshimika katika jamii.
Mandela alianza kutumikia kifungo katika jela iliyopo kwenye kisiwa cha Robben kilichopo kwenye bahari ya Atlantic umbali wa kilometa 12 kutoka mji wa Cape Town, alimotumikia kifungo kwa miaka 18, na mwaka 1982 aliondolewa ndani ya kisiwa hicho na kuhamishiwa kwenye gereza pia lenye ulinzi mkali la Pollsmoor lililopo Cape Town na siku chache kabla ya kuachiwa huru alihamishiwa gereza lililopo mjini Cape Town la Victor Verster.
Kisiwa cha Robben kwa takriban miaka 400 iliyopita kimekuwa kikitumika kama eneo la kuadhibu watu, kuweka watu katika maisha ya kuwatenga na kuwafunga jela. Ni kisiwa kwa ajili ya watu wasumbufu wa kisiasa, wasumbufu katika jamii na watu wasiotakiwa katika jamii.
Kama ilivyo kwa viongozi na wanaharakati wengine wa ukombozi wa kiafrika waliopata changamoto za Serikali za kikoloni kwa kukamatwa, ambao baadaye walikuja kushika uongozi wa nchi zao, kama vile Kwame Nkrumah wa Ghana, Jomo Kenyatta wa Kenya na Robert Mugabe wa Zimbabwe, Mandela naye alipotoka jela alikuwa Rais wa kwanza mweusi nchini Afrika Kusini.
Gereza la Kisiwa cha Robben, lililofahamika kwa jina la gereza ndani ya gereza, lilikuwa ni gereza lenye zahama na ukiwa. Kufungwa ndani ya gereza hilo maana yake ni muda mwingi kufanya kazi za suluba, lakini kulikuwa na fursa kwa mfungwa kupata muda wa kujisomea, kufanya mijadala na kujipima. Miongoni mwa masharti ya kushikilia maadili ndani ya gereza hilo ni kwa wafungwa kujikita kwenye kusoma na kufanya mijadala. Tabia ya Mandela na uongozi wenye weledi ni matokeo ya maisha ya jela au ‘Chuo Kikuu cha Kisiwa cha Robben.’
“Hakuna zaidi ya kuelekeza akili zako kwa kuwa mtulivu zaidi kwa kukubali ukweli wa jamii yako,” alisema Mandela. Mwanzoni mwa mwaka 1972, alipewa ofa ya kutoka jela kwa sharti la kutangaza kukomesha vurugu dhidi ya Serikali ya Makaburu, ofa mabayo aliikataa akisema kuwa Serikali ndiyo imekifanya chama cha ANC kutumia njia ya uanaharakati.
Maisha ya jela ndiyo yaliyombadili Mandela na kuwa kiongozi mwenye ushawishi, ambapo akiwa gerezani alijifunza kuhusu hisia za binadamu na namna ya kuondoa hofu na mambo yasiyo ya usalama kwa wengine. Akiwa gerezani Mandela aliwavutia askari magereza kwa namna alivyokuwa mtetezi wa haki, mweye heshima na mwenye uelewa wa masuala ya kisheria, ambapo ndani ya gereza la Kisiwa cha Robben alikuwa kiongozi wa wafungwa wenzake.
Kwa mujibu wa taarifa askari magereza walikuwa chini ya uongozi wa wafungwa na wafungwa walikuwa chini ya uongozi wa Mandela.
Mwandishi wa habari Eddie Koch aliandika kwenye magazeti ya Mail na Guardian kuwa selo namba saba alimokuwa akiishi Mandela, lilikuwa eneo lenye harakati nyingi za ulinzi mkali ndani ya gereza hilo kwa kila Jumamosi ya wiki.
Wakati Mandela akiwa ndani ya gereza hilo kulikuwa na mikwaruzano ya wafungwa, kutoka kitengo cha kijeshi cha ANC, chama cha Pan Africanist Congress na wanaharakati wa Steve Biko’s Black. Vurugu ndani ya gereza hilo zilifanyika kwa misingi ya kupingana watu binafsi na tofauti ya itikadi, ambapo vurugu hizo zilikuwa kipimo cha mbinu za uongozi wa kidiplomasia wa Mandela na wenzake.
Taarifa zilisema wafungwa wengi wapya walipelekwa kwenye gereza hilo la Kisiwa cha Robben, kama vile viongozi wa wanafunzi wa Soweto, wawakilishi wa baraza waliochochea vijana hadi wakaazisha vurugu nchini humo mwaka 1976, hawakuwa na ufahamu kuhusu hali ya kisiasa ndani ya gereza hilo.
Hivyo ilikuwa ni jukumu la Mandela na wenzake kuwaelimisha na kuwapa taratibu za gereza hilo wafungwa hao wapya vijana, gereza hilo lilikuwa sehemu huru kwa wasomi kutumia vipaji vyao. Gereza la Kisiwa la Robben lilijengwa kwa namna ambayo limezuia mawasiliano kati ya uongozi, askari au viongozi waandamizi wa harakati.
Wafungwa ambao ni viongozi waandamizi katika vyama vyao nje ya gereza, kila mmoja alifungwa kwenye selo yake iliyokuwa kwenye jengo B. Wahalifu sugu na wapiganaji wa msituni ambao lengo lao ni kuuondoa utawala wa makaburu waliwekwa kwenye jengo A ambalo limetengwa na majengo mengine.
Jengo G limejengwa kwa wafungwa wengi kuishi katika selo moja. Siku za nyuma wafungwa wenye asili ya Kihindi walikuwa wakitenganishwa na wafungwa wenye asili ya waafrika weusi.
Mandela siku zote alipopata fursa ya kuzungumza na askari magereza wa Afrikaner aliwataka kujielekeza kwenye mstari wa fikira za ANC. Hali hiyo ilimsaidia kujiimarisha kwa kuwa na mbinu mpya kila mara za kujenga hoja.
Hata hivyo, rafiki wa Mandela, Walter Sisuli ambaye walikuwa naye gerezani, alichukulia mazungumzo hayo kama mwanzo wa makubaliano na serikali ya kibaguzi.
Mandela pia akiwa gerezani alitumia muda huo kujiendeleza katika elimu ya sheria. Alibaini kuwa elimu hiyo inamsaidia kuweka msingi kwa makubaliano ya mwisho yasiyo ya kumwaga damu, kwa mslahi ya Afrika Kusini ijayo.
Insha na maandiko ambayo hayakuchapishwa aliyoyaandika akiwa gerezani yaliifanya Afrika Kusini iwe kama mshangiliaji, ilionyesha usomi zaidi na uasilia kuliko ule wa awali wakati wa mapambano na wakoloni. Alikuwa na matarajio ya kupata ukweli.
Mandela aliona jela kama vile maabara ya namna rangi tofauti zinaweza kuelewana na kuishi kwa utulivu. Aliona gereza kama mwakilishi wa jamii wa maelewano nchini Afrika Kusini ambayo yanaweza kudumishwa.
Hata hivyo, mkuu wa gereza Colonel Willie mwaka 1971 alizungumzia uwezo na utayari wa Mandela wa kuongoza serikali ya mpito nchini Afrika Kusini: “Mandela ana kariba ya kipekee. Amepata uzoefu wa mabadiliko ya kisiasa. Sidhani kama anasubiri kwa ajili ya kulipa kisasi. Sijaona chuki kwa yeyote miongoni mwao, lakini Mandela ana nafasi kubwa ya kuwashawishi.”
Alisema akiwa gerezani amekuwa akishirikiana na wazungu na wahindi ambapo walimuamini kwa asilimia kubwa, kwakuwa hakuwa anazungumzia kulipa kisasi kwa watu wa rangi nyingine.
Kilichompeleka jela
Mandela ambaye alikuwa kiongozi wa jumuia ya African National Congress (ANC), ambayo ilikuwa ikipinga ubaguzi wa rangi, mwaka 1956 alikamatwa kwa tuhuma za uhaini, lakini aliachiwa huru. Mwaka 1960 ANC ilipigwa marufuku na Serikali ya Makaburu.
Mwaka 1961, Mandela na viongozi wengine wa ANC waliunda jumuia nyingine iliyoitwa Umkhonto we Sizwe (MK), ambayo ilikuwa ni kitengo cha kijeshi cha ANC. Desemba 16, 1961, MK, ambayo Mandela alikuwa mkuu wake wa majeshi, kilifanya shambulio la bomu kwenye maeneo ya Serikali na walianzisha mapigano ya msituni. Mandela alikamatwa Agosti 5, 1962, na alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kwa kuchochea wafanyakazi kugoma katika mgomo wa wafanyakazi uliotokea mwaka 1961.
Julai 1963 serikali ilishambulia shamba la Lilliesleaf lililokuwa Rivonia, ambalo lilikuwa likitumiwa na ANC kama maficho yao. Viongozi 19 wa ANC walikamatwa na kukutwa na nyaraka zilizoonyesha uhusiano wao na MK na mipango ya kufanya mashambulizi ikiwemo vita vya msituni.
Serikali ya makaburu iliwafungulia mashitaka viongozi 11 wa ANC, chini ya sheria ya uhalifu wa kufanya hujuma ya mwaka 1962. Wakati wa kesi Mandela hakutaka kuwa na shahidi na badala yake alielezea historia ndefu ya malengo ya ANC na MK, ambapo alikiri baadhi ya makosa lakini alijitetea kwa kosa la kutumia vurugu kudai haki. Na Julai 1964 alihukumiwa kifungo cha maisha jela. (NMG).

Comments

Popular posts from this blog

alahh hii ni kali ya mwaka madam Martha!-3

ANGALIA PICHA ZA KANGA MOKO BALAA INYE NJE NJE!